728x90 AdSpace

Latest News

Monday, September 22, 2014

PINDA AELEZA UHALALI WA BUNGE MAALUMU LA KATIBA: SOMA HAPA ALICHOKISEMA

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda amesisitiza kuwa hakuna sababu ya msingi ya kusitisha Bunge Maalumu la Katiba kwa kuwa mchakato wake unaoendelea sasa upo kisheria na ameomba waumini wa dini na viongozi wao kuombea ili uweze kumalizika kwa usalama.

Bunge hilo Maalumu, leo linatarajiwa kuanika hadharani Rasimu ya Tatu ya Katiba mpya, ikiwa ni moja ya hatua za mwisho za kukamilisha mchakato wake, kabla ya kurudishwa kwa wananchi.

Pinda alibainisha hayo jana wakati wa ibada ya uzinduzi wa Dayosisi mpya ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Ziwa Tanganyika, kuwekwa wakfu na kusimikwa kwa Askofu wake wa kwanza, Askofu Mebele Anyigulile Mwaipopo na Msaidizi wa Askofu Mchungaji David Waramoo Masaoe.

Sherehe za ibada hiyo zilifanyika mjni Sumbawanga, mkoani Rukwa na kuhudhuriwa na mamia ya waumini, maaskofu wa Dayosisi zote za KKKT nchini wakiongozwa na Askofu Mkuu wa KKKT nchini, Dk Alex Malasusa, viongozi wa Serikali, wakiwemo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosia, Wakuu wa Mikoa ya Rukwa, Stella Manyanya na Katavi, Dk Rajab Rutengwe na viongozi wa vyama vya siasa.

Waziri Mkuu aliyasema hayo kwa staili ya kujibu msimamo wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) na Jukwaa la Wakristu Tanzania alioueleza Askofu Mwaipopo katika hotuba yake mara baada ya kuwekwa wakfu, wakitaka Bunge hilo Maalumu la Katiba lisitishwe na pia liheshimu maoni yaliyomo katika Rasimu iliyoandaliwa na Tume ya Jaji Joseph Warioba.

Mwaipopo akishangiliwa na waumini waliohudhuria ibada hiyo, alisisitiza kuwa Bunge hilo limekosa mwelekeo hivyo lisitishwe ili kutoa nafasi ya kujipanga upya, kwani kujikosoa ni ujasiri.

Waziri Mkuu Pinda katika hotuba yake, alisisitiza kuwa mchakato unaoendelea ndani ya Bunge hilo Maalumu ni halali na kwamba uko kisheria kwa vile kinachofanyika sasa ni kuiboresha Katiba.

Alilitaka Kanisa nchini kuliombea Bunge hilo Maalumu ili mchakato wake huo uweze kumalizika kwa usalama akisitiza kuwa katika mambo sita yaliyotolewa maoni na wananchi waliochangia, kulikuwa na idadi ndogo sana ya waliochangia kuhusu muundo wa Serikali.

Alisisitiza kuwa iwapo tatizo ni muundo wa Serikali basi ni bora mchakato kama ikiwezekana urejeshwe kwa wananchi ili waweze kupiga kura ya maoni waulizwe kama wanataka Muungano na wa aina gani. Katika hotuba yake hiyo, Waziri Mkuu alieleza wazi kukerwa na historia mbaya ya wakazi wa mikoa ya Rukwa na Katavi kuendekeza ushirikina,

“kutoka moyoni najaribu sana kuipiga vita tabia hii ambayo si nzuri hata kidogo,” alieleza.

Alimuomba Askofu Mwaipopo kupiga vita ya kuamini ushirikina kwa vile imekuwa chanzo cha mauaji ya watu wasio na hatia wakiwemo vikongwe na walemavu wa ngozi kunyofolewa viungo vyao.

“Mimi sijawahi kuona, lakini Baba Askofu wapo watu katika mikoa hii miwili ya Rukwa na Katavi wenye uwezo wa kutengeneza radi wakati wa kiangazi hili nalo nakuomba ulibebe kwa kuwaelimisha waumini… wewe una watu wengi… “Isitoshe inastaajabisha utakuta mabango mijini mganga wa kienyeji akijinasibu kuwa anatoka Sumbawanga eti kila mganga mahiri wa kienyeji shuruti atoke Sumbawanga hii si historia nzuri, lazima ipigwe vita, “ alibainisha.

Awali Dk Malasusa alisisitiza kuwa utunzaji wa mazingira ni suala la kibiblia, na alishangazwa na tabia ya baadhi ya viongozi nchini kutokuwa na dhamira ya dhati na kweli ya utunzaji wa mazingira.

“Katika majukwaa utawasikia wakikemea uchomaji wa misitu lakini ni hao hao wanaomiliki kampuni za ukataji miti, vivyo hivyo wanapiga vita ujangiri lakini ni hao hao wanaomiliki vitalu vya uwindaji katika Hifadhi zetu za Taifa… wanayosema ni mbali na matendo yao,“ alisititiza.

Kwa upande wa rushwa, alikemea kwa kusema kuwa baadhi ya viongozi wamekuwa mstari wa mbele kuzungumzia rushwa lakini hawana kabisa dhamira ya kuitokomeza kwa kuwa hawajatambua wajibu wao mbele za Mungu.
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 comments:

Post a Comment

Item Reviewed: PINDA AELEZA UHALALI WA BUNGE MAALUMU LA KATIBA: SOMA HAPA ALICHOKISEMA Description: Rating: 5 Reviewed By: Unknown
Scroll to Top